Wito umetolewa kwa Serikali pamoja na wadau wa maendeleo kuongeza juhudi katika utoaji wa elimu ya hedhi salama kwa watoto wa kike walioko vijijini, ili kusaidia kuondoa changamoto wanazokutana nazo wakati wa kipindi chao cha hedhi.
Wito huo umetolewa Mei 28, 2025 na Afisa Tawala Wilaya ya Mvomero Bw. Flezier Mang’ula akimuwakilisha Mkuu wa Wilaya hiyo katika maadhimisho ya Siku ya Hedhi Salama Duniani yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.
Afisa Tawala huyo amesema kuwa bado kuna uelewa mdogo kuhusu hedhi salama katika maeneo ya vijijini, ambako miradi ya kuwasaidia wasichana kutoka na hedhi haipo, hali inayosababisha aibu, unyanyapaa na hata utoro mashuleni kwa wasichana.
"…ziko jitihada zinazohitajika kwa Serikali kwa maana ya Halmashauri kwa kushirikiana na wadau ili kuweza kutoa elimu ya kuwasaidia wananchi na wanafunzi kufikia hedhi salama…” amesema Bw. Mang’ula.
Aidha, amelipongeza shirika la AfriCraft kupitia mradi wao wa Binti ambao unatoa elimu na mafunzo ya utengenezaji wa taulo za kike za kufua kwa wanafunzi na walimu wa Vyuo vya Ufundi Stadi (VETA DAKAWA, VETA KIHONDA) Pamoja na shule za sekondari za Mvomero, Sokoine Memorial na Wami Dakawa.
Naye, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero Dkt. Phillipina Phillipo amesema Serikali inaendelea kuboresha miundombinu ya shule ambapo inajenga vyoo vyenye vyumba maalum kwa ajili ya wasichana kujisitili wakati wa hedhi pamoja na kutoa taulo za kike za kisasa kwa kila shule.
Kwa upande wake, Meneja Miradi ya Afya kutoka Shirika la AfriCraft ambalo linatekeleza mradi wa Binti Bi. Aneth Kiyao amesema kuwa hadi sasa wamefanikiwa kuwafikia wasichana zaidi ya 35000 ambao wamepatiwa taulo za kike, Wavulana 18000 ambao wamepatiwa elimu ya hedhi na usawa wa kijinsia.
Akizungumza kwa niaba ya wasichana waliopata elimu na mafunzo juu ya hedhi salama, Mwanafunzi Anastazia Sunday kutoka shule ya Sekondari Mvomero amesema kupitia mradi huo umesaidia kupunguza utoro kwa wasichana ambao walikuwa hawafiki shule wakati wa hedhi.
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.