Jumla ya miche 2140 ya mikarafuu imetolewa kwa wanafunzi 214 wa kidato cha kwanza katika Shule za Sekondari za Mongola na Mgeta Wilayani Mvomero ambapo kila mwanafunzi amepewa miche 10 kwenda kupanda katika maeneo yao ikiwa ni njia ya kuwainua kiuchumi na kuwasaidia wanafunzi hao kutimiza ndoto zao za kusoma hadi chuo kikuu.
Zoezi hilo limefanyika Mei 13, 2025 likiongozwa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro Alhaji Dkt. Mussa Ali Mussa wakati wa ziara yake ya kikazi katika Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero inayolenga kuwajengea wanafunzi msingi wa kujitegemea kiuchumi kupitia kilimo cha mikarafuu.
Katibu Tawala huyo amesema Wanafunzi watakaonufaika na kampeni ya "JISOMESHE NA MKARAFUU" Mkoani humo ni wanafunzi wa kidato cha kwanza wa kila mwaka watapewa miche hiyo ili kuwawezesha wanafunzi hao kujikwamua kiuchumi pamoja na kuweza kulipa ada za shule na chuo watakapofika elimu ya juu hivyo kutokuwa tegemezi kwa wazazi wao ama mikopo inayotolewa na Serikali.
"Karafuu ina matumizi mengi, na ikitunzwa vizuri, inaweza kuwa msaada mkubwa kwa maisha ya baadaye ya hawa watoto, Tunawalea vijana watakaojitegemea," amesema Dkt. Mussa
Sambamba na hayo, Dkt. Mussa amewaelekeza walimu na jamii kwa ujumla kupanda miche ya zao la mikarafuu katika maeneo ya shule na hata nyumbani, ili kuendeleza utamaduni wa kutumia rasilimali kilimo kama nyenzo ya kukuza elimu na kupambana na umasikini.
Pamoja na ugawaji huo wa miche, wanafunzi wamepatiwa elimu ya utunzaji wa miche hiyo, ikiwemo kuchagua maeneo sahihi ya kupanda, kuitunza kwa maji na mbolea na kujifunza umuhimu wa kuvumilia hadi kipindi cha kuvuna zao hilo.
MWISHO
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.