Serikali ya Wilaya ya Mvomero imeanza kuchukua hatua madhubuti za kutatua mgogoro wa ardhi uliodumu kwa muda mrefu katika Kijiji cha Doma, kwa lengo la kurejesha amani, mshikamano na haki kwa wananchi.
Hatua hiyo imeelezwa Februari 11, 2026 na Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Mhe. Maulid Dotto, wakati wa kikao maalum kilichofanyika kijijini hapo, kilichowakutanisha viongozi wa kijiji, wananchi na wataalamu kutoka sekta ya ardhi.
Mhe. Dotto amesema kuwa serikali imejipanga kikamilifu kuhakikisha mgogoro huo unamalizika kwa njia ya haki na kwa kuzingatia sheria, taratibu na maslahi ya wananchi wote.
Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya, amesisitiza umuhimu wa kuwatambua rasmi wananchi wote waliopo katika eneo la mgogoro, ili kuwezesha serikali kupata takwimu sahihi zitakazosaidia katika upangaji na utoaji wa maamuzi ya kudumu. Ameongeza kuwa zoezi hilo litahusisha uhakiki wa umiliki wa ardhi, mipaka ya shamba pamoja na nyaraka halali za umiliki.
Kwa upande wake, Afisa Ardhi wa Wilaya Bw. Charles Wandwi ameeleza kuwa timu ya wataalamu ipo tayari kufanya kazi ya uhakiki wa maeneo husika, huku wananchi wakihimizwa kutoa ushirikiano kwa kutoa taarifa sahihi na kujitokeza wakati wa zoezi hilo.
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero Mhe. Koila Majuka ameelza kuwa Waheshimiwa Madiwa kwa kushirikiana na Timu ya Mkuu wa Wilaya watahakikisha wananchi wanapata haki yao Pamoja na mwenyekezaji naye anapata haki yake.
Diwani wa Kata hiyo ya Doma amemshukuru Mkuu wa Wilaya kwa kuchukua hatua ya kutatua mgogoro huo huku akisisitiza kuwa zoezi la uhakiki lifanyike kwa uwazi.
Wananchi wa Kijiji cha Doma wameishukuru serikali kwa kuchukua hatua za haraka na kuahidi kushirikiana kikamilifu katika zoezi la utatuzi wa mgogoro huo, wakieleza matumaini yao kuwa suluhisho la kudumu litapatikana na kuondoa migogoro ya mara kwa mara iliyokuwa ikikwamisha maendeleo ya kijiji hicho.
MWISHO.
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.