Wananchi wapatao 9,254 wa Wilaya ya Mvomero wanatarajia kunufaika na mpango wa Bima ya Afya kwa Wote katika awamu ya kwanza, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliyoitoa wakati wa Kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani uliofanyika Oktoba 29, 2025.

Akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa zoezi la uhakiki, usajili na ugawaji wa kadi za bima iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri Februari 13, 2026, Katibu Tawala wa Wilaya hiyo Ndg. Said Nguya amesema mpango huu ni sehemu ya jitihada za Serikali kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora za afya bila vikwazo vya kifedha huku akieleza kuwa mpango huu unalenga kuwafikia wananchi wote, hususan wa kipato cha chini, ili kuimarisha ustawi wa jamii.

Kwa upande wake, Afisa Uanachama Mwandamizi kutoka Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoa wa Morogoro Bi. Rosemilia Msigwa amebainisha kuwa kwa Wilaya ya Mvomero pekee jumla ya Kaya 2,106 zenye wakazi 9,254 zitasajiliwa na kupatiwa kadi za bima kwa awamu ya kwanza akiongeza kuwa Serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni 315,900,000 kwa ajili ya bima. Aidha, ameongeza kuwa Bima hiyo itawawezesha kupata huduma katika vituo vyote vya kutolea huduma za afya vya Serikali.


Naye, Mganga Mkuu wa Halmashauri hiyo Dkt. Phillipina Phillipo ameeleza kuwa Idara ya Afya imejipanga kuwapokea na kuwahudumia wanachama wapya wa bima ya Afya, akiongeza kuwa maandalizi yamefanyika ikiwemo ya kuboresha huduma kwa kuongeza watoa huduma, vifaa tiba Pamoja na kusajili vituo vyote katika mfumo wa bima unaoratibiwa na Mamlaka ya usimamizi wa bima Tanzania – TIRA.



Nao, wananchi waliopatiwa bima hiyo wameeleza kufurahishwa na hatua hiyo, wakisema itapunguza gharama za matibabu na kuwawezesha kupata huduma kwa wakati, wakiongeza kuwa awali walikuwa wakikumbwa na changamoto ya kugharamia matibabu, hali iliyokuwa ikiathiri maisha yao na familia zao.



MWISHO.
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.