Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero imetangaza rasmi kuanza kwa mauzo ya zao la ufuta kupitia mfumo wa Stakabadhi Ghalani kuanzia Mei 20, 2025, hatua inayolenga kuhakikisha wakulima wananufaika kwa kupata bei nzuri ya mazao yao.
Hayo yamebainishwa Mei 16, 2025 na Katibu Tawala Wilaya ya Mvomero Ndg. Said Nguya wakati wa kikao cha Wadau wa Stakabadhi za Ghala kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ambapo wajumbe wa kikao hicho wameunga mkono azimio hilo.
Katibu Tawala huyo amewataka Waheshimiwa Madiwani, Watendaji wa Kata na Vijiji, Maafisa Ushirika na Maafisa Ugani pamoja na wataalam wa kilimo kushirikiana kutoa elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa Mfumo huo na kuwahamasisha kuutumia ili waweze kupata faida ambayo wamekusudia kuipata.
"...kwa hiyo kikao hiki tunakubaliana kwamba zao la ufuta kwenye stakabadhi ya ghala tunaanza rasmi tarehe 20 mwezi wa tano..." amesema Ndg. Said Nguya.
Aidha, pamoja na azimio hilo wajumbe wa kikao hicho wameadhimia kuongeza vituo vya ukusanyaji wa mazao katika maeneo ambayo yanachangamoto ya maghala ili kudhibiti walanguzi wa mazao ya wakulima.
Sambamba na hilo, Wajumbe wameazimia kuwa Maafisa Ushirika wahamasishe wakulima kujiunga katika vyama vya Ushirika katika Tarafa za Mlali na Mgeta.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Bi. Loema Peter amewataka Maafisa Ushirika, Maafisa ugani, kilimo pamoja na watendaji wa Kata na Vijiji kuhakikisha kuwa wanafanikisha suala hilo huku akiwataka kila mmoja kuwajibika katika nafasi zao.
Ameongeza kuwa hadi kufikia siku ya jumatatu maandalizi muhimu yatakuwa yamekamilika huku akisema kuwa wananchi watapatiwa elimu ili wawe na uelewa na mfumo huo.
Akielezea mikakati ya Halmashauri katika kuongeza uzalishaji wa zao la kakao, Afisa Ushirika wa Halmashauri hiyo Bw. Mihayo Lukaya amesema kuwa Halmashauri imeweka mikakati ya kuanzisha kitalu cha miche ya kakao 100,000 kila mwaka, ambapo hadi sasa miche 12, 254 imezalishwa na kugawanywa bure kwa wakulima wa Kata za Mhonda, Kweuma, Sungaji, Diongoya na Maskati.
MWISHO
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.