Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Mhe. Judith Nguli ametoa mbinu kwa wananchi wa Wilaya ya Mvomero ili kujiepusha na athari za tembo wanaovamia mashamba ya wananchi hao kwa kula mazao na kuwasababishia hasara kubwa kwenye mavuno.
Ameyasema hayo alipofanya ziara na kufanya mkutano wa hadhara katika Vijiji vya Kimbambila, Kata ya Lubungo na Kibaoni, Kata ya Melela, Msongozi kata ya Msongozi na Kijiji cha Mlandizi kata ya Manga alipofika na kupokea malalamiko ya wananchi juu ya adha wanazopitia kwa mashamba yao kuvamiwa na tembo mara kwa mara na kufanya uharibifu unaosababisha hasara kiuchumi kwa wananchi hao.
Mkuu wa Wilaya amewataka wananchi kulima zao la Ufuta kwani zao hilo kiutalaamu limeonekana kuepukwa kuliwa na wanayama aina ya tembo tofauti na mazao mengine kama mahindi na athari ya uharibifu inayotokana kilimo cha zao hilo ni ndogo sana. Amewaasa wananchi wanapolima mzao mengine, wasisahau kulima na ufuta kwani tembo wameonekana kutokula zao hilo.
“Naomba mnapolima mazao mengine kama mahindi, changanyeni na zao la ufuta. Tembo watakapovamia shamba lako, hawatakula ufuta, wataishia kuukanyaga tu. Watakula mazao mengine ila utapunguza hasara ambayo ungeipata kama ungelima mahindi peke yake.”, amesema Mkuu wa Wilaya. Amewaasa wananchi hao kulima walau ekari moja au mbili kama majaribio ili waone faida yake. Ameongeza kuwa ufuta ni zao la biashara lenye soko sana kwa sasa hivyo wananchi watajikwamua kiuchumi pindi watakapolima zao hilo.
Katika hatua nyingine, Mkuu wa Wilaya amewataka wananchi kutoingiza mifugo kwenye hifadhi kwani kufanya hivyo ni sababu moja inayofanya tembo kutoka kwenye hifadhi na kuingia kwenye makazi ya wananchi.
Kuhusu mauaji na majeruhi yanayosababishwa na uvamizi wa tembo, Mkuu wa Wilaya amewahakikishia Wananchi kuwa Serikali inafanya jitihada kuongeza Askari Wanyamapori huku akisema kuwa tayari wana makubaliano ya pamoja kati ya TANAPA, TAWA pamoja Halmashauri kuongeza vijana ambao tayari wameshapewa mafunzo ya udhibiti na watapewa ajira ili kuongeza nguvu na kupunguza adha ya tembo kwa wananchi.
Mkuu wa Wilaya pia amewataka wanachi wenyewe kuchukua tahadhari na waache kutembea wenyewe hasa nyakati za usiku kwani amepokea visa vingi sana vya wananchi kuuliwa na tembo katika kata zinazopakana na Hifadhi ya Taifa ya Mikumi.
Katika hatua nyingine, Mkuu wa Wilaya amewataka wananchi waishio kwenye maeneo hayo kuanzisha Jumuiya ya Hifadhi za Wanyamapori (WMA) kwani kuna faida za uchumi zinazopatikana kutoka kwa wafadhili na fedha zinazopatikana kutokana na ufadhili wa uhifadhi wa meneo hayo inaweza kutumika kwenye huduma mbalimbali za kijamii kama ujenzi wa Zahanati au Vituo vya Afya.
Shughuli za kibinadamu katika Kata za Doma, Msongozi, Mangae, Lubungo na Melela katika tarafa ya Mlali wilaya ya Mvomero zinaathiriwa sana na tembo ikiwa ni pamoja na kuharibu mashamba inayowarudisha nyuma kiuchumi pamoja na kusababisha ulemavu na vifo kwa vipindi mbalimbali.
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.