Mkurugenzi wa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Ndg. Ramadhani Kailima ametoa wito kwa waandishi wasaidizi na waendesha vifaa vya bayometriki ngazi ya kituo wilayani Mvomero kuhakikisha wanazingatia muda wa kufungua vituo vya kuandikisha wapiga kura ili kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wananchi.
Ndg. Kailima ametoa wito huo Mei 14, 2025 wakati akizungumza na washiriki wa Mafunzo ya zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga kura Awamu ya Pili yaliyofanyika katika ukumbi wa Prof. Kuzilwa uliopo katika Kata ya Mzumbe.
Mkurugenzi huyo amesema kuwa uchelewaji wa kufungua vituo unaweza kuwakatisha tamaa wananchi na kudhoofisha hamasa ya kushiriki katika mchakato wa uchaguzi.
Aidha, ameongeza kuwa Tume ya Uchaguzi imejipanga kuhakikisha zoezi hilo linafanyika kwa uwazi, ufanisi na kwa kuzingatia maadili ya uchaguzi, na kwamba usimamizi wa karibu katika kila ngazi ni muhimu ili kuhakikisha lengo hilo linafikiwa.
Sambamba na hilo, Mkurugenzi huyo amewasisitiza washiriki hao juu ya umuhimu wa kutunza vifaa ambavyo vinatumika katika zoezi hilo akisema kuwa vifaa hivyo vimenunuliwa kwa gharama hivyo wanapaswa kuvitunza.
Kwa upande wake Afisa Muandikishaji Daftari la kudumu la wapiga kura Jimbo la Mvomero Bi. Mary Kayowa amesema kuwa katika zoezi la uboreshaji wa Daftari la kudumu la wapiga kura awamu ya pili Jimbo hilo litakuwa na vituo 50 ambavyo vitatumika akiongeza kuwa zoezi hilo litafanikiwa kwa asilimia 100 kwa kuwa hamasa kwa wananchi inaendelea kufanyika.
Aidha, Bi. Mary Kayowa amewataka washiriki kuwa na ushirikiano pamoja na kufanya kazi kwa weledi ili kuhakikisha kuwa malengo yaliyowekwa na Tume yanafikiwa.
Zoezi la uboreshaji wa Daftari la Kudumu la wapiga kura kwa Awamu ya Pili linatarajia kuanza tarehe 16 hadi 22 Mei, 2025 huku likienda sambamba na kuwekwa wazi kwa Daftari la Awali.
"Kujiandikisha kuwa Mpiga Kura ni Msingi wa Uchaguzi Bora".
MWISHO.
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.