Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Mhe. Judith Nguli, ametimiza ahadi yake ya kugharamia matibabu ya kijana Ramadhani Mohamed (20) mkazi wa Kichangani katika Tarafa ya Turiani ambaye amekuwa akisumbuliwa na maradhi ya mguu kwa muda mrefu.
Akizungumza leo Aprili 28, 2025 wakati akikabidhi fedha kiasi cha shilingi laki 8 huku akishuhudia kijana huyo akipelekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mvomero kwa ajili ya kuanza matibabu ya awali, DC Nguli amesema kuwa Serikali ina dhamira ya dhati ya kuhakikisha wananchi wote, hususan vijana, wanapata huduma bora za afya bila vikwazo.
"...kama Mkuu wa Wilaya kwa niaba ya Serikali ilichukua changamoto hile na kuipeleka Serikalini...tunamshukuru Mhe. Rais kwa namna ambavyo ametusaidia katika kuhakikisha anatoa matibabu ya mtoto huyu Ramadhani Mohamed..." amesema Mhe. Nguli.
Mkuu huyo wa Wilaya amesema kuwa hatua hiyo inaonesha dhamira dhati ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuwahudumia wananchi kwa vitendo, hasa katika sekta muhimu kama afya.
Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya amewashukuru wadau mbalimbali wakiwemo SAT ambao wamechangia kiasi cha shilingi laki 8 kwa ajili ya kufanikisha matibabu ya mtoto huyo ambapo kiasi cha shilingi laki tano na ishirini itatumika kwa ajili ya bima na kiasi kinachobakia kwa ajili ya gharama nyingine za matibabu.
Ameongeza kuwa kijana huyo ataanza kuhudumiwa na Hospitali ya Wilaya wakati wakisubiri Kambi ya madaktari bingwa wa Mama Samia katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro ambayo inatarajiwa kuanza tarehe 5 hadi 16 mwezi Mei 2025.
Ramadhani Mohamed, ambaye anasumbuliwa na matatizo ya mguu wa kulia alikosa uwezo wa kifedha wa kupata huduma maalum za matibabu hivyo Mhe. Judith Nguli alichukua jukumu la kumsaidia baada ya kuguswa na hali yake katika moja ya mikutano ya hadhara.
Akitoa neno la shukrani kwa Serikali Baba mkubwa wa kijana Ramadhani Bw. Amini Juma Hussein Mkazi wa Kichangani, Tarafa ya Turiani ameishukuru Serikali Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kufanikisha matibabu ya kijana huyo.
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.