Waheshimiwa Madiwani katika Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero wametakiwa kuongeza kasi ya ufuatiliaji na usimamizi wa karibu wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yao ili kuhakikisha inatekelezwa kwa ubora, kwa wakati na kwa kuzingatia thamani ya fedha (Value for money) inayotolewa.

Wito huo umetolewa Januari 9, 2026 na Katibu Tawala Wilaya ya Mvomero Ndg. Said Nguya wakati akifungua rasmi mafunzo elekezi kwa Waheshimiwa Madiwani ikiwa ni siku ya pili ya mafunzo hayo ambayo yanafanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri.

Katibu Tawala huyo ameeleza kuwa madiwani wana nafasi muhimu ya kusimamia miradi hiyo kwa kuwa inatekelezwa katika maeneo yao akiongeza kuwa ufuatiliaji wa karibu wa miradi utasaidia kubaini changamoto mapema na kuzitatua kwa wakati na kuzuia ubadhirifu wa fedha za umma unaoweza kujitokeza, sambamba na kuongeza uwajibikaji kwa wakandarasi na wasimamizi wa miradi.
“...niwaombe sana miradi inayotekelezwa kule kwenye maeneo yenu sisi ndiyo tuwe jicho la kwanza kabla ofisi ya Mkuu wa Wilaya na usalama haijakwenda kugundua mapungufu ambayo yapo kwenye mradi...” amesema Katibu Tawala.
Aidha, Katibu Twala huyo amewahimiza kushirikiana kwa karibu na Wataalam wa Halmashauri, watendaji wa kata na vijiji huku akiwasisitiza kuepuka migogoro isiyo na lazima.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero Mhe. Koila Korman Majuka ameishukuru Serikali inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuruhusu madiwani hao kupata mafunzo ambayo yatasaidia kuwaletea maendeleo wanamvomero.
Naye, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ameeleza kuwa mafunzo hayo ya siku tatu yanatarajiwa kuhitimishwa Januari 10 akiongeza kuwa mada mbalimbali zitatolewa ambazo zitawasaidia waheshimiwa madiwani kutekeleza majukumu yao.
MWISHO
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.