Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Mussa Ali Mussa ameendelea na kampeni ya Jisomeshe na Mkarafuu Wilayani Mvomero, ikiwa na lengo la kuwawezesha wanafunzi kiuchumi kupitia kilimo cha mkarafuu ambapo leo Machi 14, 2025 amegawa miche ya mikarafuu kwa wanafunzi wa kidato cha kwanza wa shule za sekondari Kipera na Homboza.
Akizungumza wakati wa zoazi la ugawaji wa miche hiyo, Dkt. Mussa amesema Viongozi wa Mkoa wa Morogoro wameanzisha kampeni hii ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuwaandaa vijana kwa maisha ya baadaye kwa kuwawezesha wanafunzi hao kujiendeleza kimasomo kupitia zao hilo.
Aidha, ameongeza kuwa miche hiyo wanapewa wanafunzi wakapande katika maeneo yao na si maeneo ya shule huku akisema kuwa kila mwanafunzi wa kidato cha kwanza atapewa miche 10 akisisitiza kuitunza ili iweze kuleta matokeo yaliyokusudiwa.
"...nyie wanafunzi wa form one, tunataka kila mwanafunzi mmoja leo hii, tumuachie miche ya mikarafuu kumi... miche hii isiwe mali ya shule mkaipande kwenu..." amesisitiza Dkt. Mussa
Kwa mujibu wa Katibu Tawala huyo, kwa sasa bei ya kilo moja ya karafuu ni shilingi 20,000/= hivyo, mche mmoja una uwezo wa kuzalisha kilo tano huku akisema kuwa kwa miche hiyo 10 itazalisha kilo 50 ambazo ni sawa na shilingi 1,000,000/= hivyo, wanafunzi wataweza kupata kipato na kusaidia gharama za masomo yao hapo baadaye
Kwa upande wake Katibu Tawala Msaidizi Sehemu ya Uchumi na Uzalishaji kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt. Rozaria Rwegasira amesema kuwa kampeni hiyo ilizinduliwa rasmi katika Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, imeendelea kutekelezwa katika Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro na sasa ipo Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero, huku akiwataka wanafunzi kuipokea kampeni hiyo ambayo itawasaidia kutimiza ndoto zao.
Naye, Mwl. Isakwisa Asesisye akimuwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero amemshukuru Katibu Tawala huyo kwa kuanzisha kampeni hiyo katika Halmashauri hiyo huku akisema kuwa Halmashauri hiyo ina jumla ya shule za sekondari 37 ambapo kwa kuanzia kampeni hiyo imeanza kwa shule za Homba na Kipera.
MWISHO
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.