Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa afua za lishe, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali kuhakikisha afya bora kwa watoto, kina mama wajawazito na jamii kwa ujumla, pamoja na kutokomeza tatizo la utapiamlo na udumavu.
Akizungumza katika kikao cha Kamati ya Lishe ya Wilaya kilichofanyika leo Disemba 15, 2025 katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo Ndg. Paulo Faty amesema halmashauri imejipanga vyema kwa kutenga bajeti maalum ya lishe kila mwaka, sambamba na kuimarisha usimamizi na ufuatiliaji wa afua huzo katika ngazi ya kata na vijiji.
Amesema miongoni mwa mikakati iliyowekwa ni kuendelea kutoa elimu ya lishe bora kwa jamii, kuhamasisha matumizi ya vyakula vyenye virutubisho, kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto pamoja na kuhimiza usafi wa mazingira ili kuzuia magonjwa yanayochangia utapiamlo.
Naye, Mganga Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Dkt. Phillipina Phillipo amesema kikao hicho kimelenga kujadili taarifa za utekelezaji wa shughuli za lishe kwa robo ya kwanza kipindi cha Julai - Septemba 2025.
Kwa upande wake Afisa Lishe wa Wilaya Bi. Niyonzima Bwenzi amesema kuwa kwa robo ya kwanza Halmashauri ilipanga kutoa kiasi cha shilingi milioni 19,698,750 ambapo fedha zilizotolewa ni shilingi milioni 36 ambayo ni sawa na asilimia 184. ameongeza kuwa kupitia kampeni ya Mwezi wa Afya na Lishe jumla ya watoto 56188 walipatiwa Vitamini A kati ya watoto 52840.
Akieleza hali ya utoaji wa chakula shuleni kwa shule za Sekondari Bw. Jaribu Marambugi akimuwakilisha Mkuu wa Divisheni ya Elimu Sekondari amesema Wilaya hiyo ina jumla ya shule za Sekondari 34 zenye wanafunzi 20171 ambapo kati yao wanafunzi 12506 sawa na asilimia 62 wanakula shuleni.
Kwa upande wa Divisheni ya elimu ya Awali na Msingi Bi. Aziza ameeleza kuwa idara imetenga kiasi cha shilingi milioni 1,600,000 kwa ajili ya kutekeleza afua za lishe kwa shule za msingi katika Wilaya hiyo.
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.