Mkoa wa Morogoro umeandaa mkakati madhubuti wa kushughulikia madai ya wafanyakazi yakiwemo madai ya likizo, uhamisho, matibabu, kukaimu, kujikimu, ajira mpya na malimbikizo ya mishahara kwa waliondolewa kazini kimakosa mwaka 2017 ili kuhakikisha kuwa wanapata stahiki zao kwa mujibu wa sheria.
Hayo yamebainishwa Mei 01, 2025 na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Kighoma Malima wakati akizungumza na Viongozi pamoja na wafanyakazi wa Mkoa huo kwenye maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi duniani (Mei Mosi) ambayo kimkoa yameadhimishwa katika uwanja wa Jamhuri, Manispaa ya Morogoro.
Mkuu huyo wa Mkoa amesema kuwa Ofisi yake itafanyia kazi suala la madai ya wafanyakazi ili kuhakikisha kuwa kila mfanyakazi anapata maslahi yake ambayo yapo kwa mujibu wa sheria.
“...baada ya Maadhimisho haya Ofisi yangu itafanya kazi ya ziada kuhakikisha kuwa suala hilo linapewa uzito wa kipekee...” amesema Mkuu wa Mkoa.
Aidha, amewataka waajiri wote Mkoani humo kuweka madai ya wafanyakazi kwenye mpango na bajeti ili kulipa madai hayo huku akisisitiza kuwa madai yao si suala la utashi binafsi bali ni takwa la kisheria.
Sambamba na hilo, Mhe. Malima amewaelekeza Waajiri kwa kushirikiana na vyama vya wafanyakazi kuhuisha orodha ya madai ya wafanyakazi na kuiwasilisha taarifa hiyo katika ofisi yake.
Kwa upande wake Mratibu wa Maadhimisho ya Mei Mosi 2025 Mkoa wa Morogoro wakati akisoma Risala iliyoandaliwa na Vyama vya wafanyakazi Mkoani humo ameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuboresha maslahi ya wafanyakazi hapa nchini.
Pamoja na pongezi hizo amemuomba Mkuu wa Mkoa kuingilia kati madai ya wafanyakazi ili waweze kupata maslahi yao.
Sherehe za Mei Mosi 2025 zinapambwa na kaulimbiu isemayo “Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025, utuletee Viongozi wanaojali Maslahi ya Wafanyakazi, Sote Tushiriki”
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.