Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Mh.Albinus Mugonya,amewataka wananchi wa Wilaya hiyo kujenga nyumba imara na zenye ubora ili kukabiliana na majanga makubwa kama vile mvua,na upepo mkali pindi yanapojitokeza.
Mkuu wa Wilaya ameyasema hayo hapo jana alipokuwa akipokea na kugawa vifaa vya msaada vilivyotolewa na ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo na Benki ya NMB kwa ajili ya wananchi walioathirika na maafa ya mvua na upepo mkali, yaliyotokea hivi karibuni katika vijiji vya Kipera na Kinyenze vilivyopo katika Kata ya Mlali,Tarafa ya Mlali na kuacha jumla ya Kaya sabini na sita (76) zikiwa hazina mahali pa kuishi.
Mkuu wa Wilaya amesema ni vyema wananchi kujenga utamaduni wa kujenga nyumba bora na imara ‘’Wananchi wanatakiwa kujenga nyumba imara ili kukabiliana na majanga kama haya yaliyojitokeza,kwani wangejenga nyumba zenye msingi imara haya yote yasingejitokeza’’ alisema.
Miongoni mwa vifaa vilivyotolewa na ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji na kukabidhiwa kwa Mkuu wa Wilaya kwa ajili ya kuvigawa kwa waathirika hao ni Unga Kilo 764, Maharagwe Kilo 100 na Chumvi Kilo 60.Wakati huo benki ya NMB imekabidhi Magodoro 54,Mashuka 108 na Mchele Kg 540 pamoja na Mafuta lita 160,na Sukari Kilo 110.
Mkuu wa Wilaya amewashukuru wadau hao kwa kuona umuhimu wa jambo hilo na kuwataka walengwa kuvigawa vifaa hivyo kwa kufuata utaratibu uliowekwa bila upendeleo wa aiana yoyote pia ametoa wito kwa wadau wengine kujitokeza kusaidia kwani waathirika wanahitaji kuendelea kusaidiwa.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Maafa Ndugu Seif Msangi Kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji,amesema kuwa miongoni mwa athari kubwa zilizosababishwa na maafa hayo ni pamoja na nyumba kuezuliwa,Vifaa pamoja na vyakula kuharibika,na kuacha uharibifu mkubwa mali na makazi ya wananchi hao.
Akipokea msaada huo kwa niaba ya Wananchi Diwani wa Kata hiyo Mh.Frank Mwananziche amesema anamshukuru Mh.Mkuu wa Wilaya na wadau kwa ujumla kwa msaada walioutoa kwani utawasaidia wananchi wake katika kipindi hiki kigumu na kuomba wadau wengine kujitokeza kutoa msaada Zaidi ya hali na mali.
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.