Mkuu wa Wilaya ya Mvomero Mhe. Judith Nguli amepiga marufuku tabia ya Watendaji wa Kata na Vijiji , Wenyeviti wavijiji kuzunguka na mihuri kwani utaratibu huo ni kinyume na sheria na kwamba mtedanji yoyote atakayebainika kuendelea na utaratibu huo , hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.
Mkuu wa Wilaya ameyasema hayo katika muendelezo wa ziara alizofanya katika tarafa ya Turiani ili kujiridhisha matumizi sahihi ya fedha za Serikali zinazoletwa kwenye miradi ya maendeleo katika shule, zahanati , vituo vya afya na miradi mbalimbali ya ujenzi katika Wilaya ya Mvomero.. Aliongeza kuwa amebaini kuwa mihuri mingi inatumika kinyume na utaratibu na kwamba tabia hiyo inawanyima wananchi wengi haki yao.
Katika hatua nyingine , Mkuu wa Wilaya ametembelea na kufanya ukaguzi katika Shule za Sekondari Kweuma, Lusanga na kukagua ukamilishwaji wa vyumba vya madarasa shule ya Msingi Difinga ambazo zote zimepata ufadhili wa mradi wa BOOST unaofadhiliwa na Kampuni ya Uchimbaji dhahabu Barrick. Pia Mkuu wa Wilaya ametembelea na kukagua ujenzi wa nyumba ya mwalimu katika shule ya Msingi Kaole , Kata ya Kanga.
Katika ukaguzi huo, amewaasa wasimamizi wa miradi hiyo waongeze kasi ya ujenzi kwani shule hizi zinategemea kuchukua wanafunzi wanaopata adha ya kutembea umbali mrefu kutafuta elimu na ni vizuri kuwatendea haki wanafunzi hao kwa kuwasogezea huduma mapema.
Akijibu swali la mwananchi aliyegusia changamoto ya upatiknaji wa mawasiliano katika Kijiji cha Difinga, Mkuu wa Wilaya amewahakikishia wananchi hao kuwa tayari Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan ameliona hilo na tayari ameingia mkataba wa ujenzi wa minara 758 ambapo mchakato wake ukikamilika vijiji vyote vyenye changamoto vitaweza kufikiwa na mawasiliano.
Awali katika ziara yake Mhe. Mkuu Wilaya alifika kukagua ujenzi wa tanki la maji katika kijiji cha Luwamba Kata ya Mhonda ambao unategemewa kusambaza maji katika vijiji vingi vya Tarafa ya Turiani na kuwaondolea adha wananchi wengi ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakikosa huduma hiyo muhimu katika kaya zao.
Huu ni muendelezo wa ziara za kikazi ambazo Mkuu wa Wilaya amejiwekea kila wiki kuwafikia wananchi na kukagua shughuli za maendeleo ambazo Serikali imekuwa ikileta fedha kuwaletea maendeleo wananchi wake.
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.