Mkuu wa Wilaya ya Mvomero, Mhe. Maulid Dotto, amezuia rasmi uuzaji wa eneo la kijiji lililopo katika Kitongoji cha Majengo, Kata ya Mlali ambapo imebainika kuwa eneo hilo limeuzwa kinyume na taratibu za kisheria, na kutoa agizo kwa uongozi wa kijij cha Kipera kuhakikisha mnunuzi wa eneo hilo anarudishiwa fedha zake mara moja.
Agizo hilo ametoa Disemba 18, 2025 kwenye mkutano wa kijiji hicho, ambapo wananchi wametoa taarifa juu ya uuzaji holela wa ardhi ya kijiji bila kufuata kanuni za usimamizi wa ardhi, na bila kupata ridhaa ya mkutano mkuu wa kijiji kama sheria inavyoelekeza.
Akizungumza mbele ya wananchi, Mhe. Dotto ameeleza kuwa ardhi ya kijiji haiwezi kuuzwa kiholela na mtu au kikundi cha watu, bali maamuzi lazima yafanywe na serikali ya kijiji kwa kushirikisha mkutano mkuu. Ameongeza kuwa ametoa agizo kwa Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Wilaya kufanya uchunguzi ili hatua za kisheria zichukuliwe kwa wale watakaobainika kuhusika kwenye mpango huo.
“…nimesitiza uuzaji huo na fedha zilizolipwa kwa ajili ya eneo hilo zirudi kwa mwenyewe…” amesema Mkuu wa Wilaya.
Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya amewataka wananchi kuendelea kuchangia fedha za ujenzi wa zahanati ya Kijiji cha Kipera ambapo ujenzi wake umefikia hatua ya lent ana tayari Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa fedha kiasi cha shilingi milioni 50 kwa ajili ya hatua ya umaliziaji wa Zahanati hiyo.
Wananchi wa kijiji hicho waliipongeza serikali ya wilaya kwa hatua hiyo, wakisema imekuja wakati muafaka kutokana na matukio ya mara kwa mara ya baadhi ya viongozi na watu binafsi kuuza ardhi kinyume cha utaratibu
MWISHO.
Wami Sokoine, Dakawa, Mvomero
Anwani Ya Posta: P.O BOX 663, MOROGORO
Msaada wa Kiufundi: +255 23 293 4348
Mobile: +255 23 293 4348
Baruapepe: ded@mvomerodc.go.tz
Hakimiliki ©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero.Haki zote zimehifadhiwa.